Na ili mumwombe msamaha Mola wenu Mlezi, kisha mtubie kwake. Atakustarehesheni
starehe nzuri mpaka muda maalumu. Na atampa kila mwenye fadhila, fadhila yake.
Na ikiwa mtakengeuka basi mimi nakukhofieni adhabu ya hiyo Siku Kubwa.
Hebu angalia! Ati wanafunika vilivyomo vifuani mwao ili wamfiche Mwenyezi Mungu!
Jueni kuwa wanapo jigubika nguo zao Yeye anajua wanayo yaficha na wanayo
yatangaza. Hakika Yeye ni Mjuzi wa yaliyomo vifuani.
NA HAKUNA mnyama yoyote katika ardhi ila riziki yake iko kwa Mwenyezi Mungu.
Naye anajua makao yake na mapitio yake. Yote yamo katika Kitabu chenye
kubainisha.
Na Yeye ndiye aliye ziumba mbingu na ardhi katika siku sita. Na Kiti chake cha
Enzi kilikuwa juu ya maji, ili akufanyieni mtihani ajuulikane ni nani miongoni
mwenu mzuri zaidi wa vitendo. Na wewe ukisema: Nyinyi hakika mtafufuliwa baada
ya kufa; wale walio kufuru husema: Hayakuwa haya ila ni uchawi uliyo wazi.
Na tukiwacheleweshea adhabu mpaka muda ulio kwisha hisabiwa wao husema: Nini
kinacho izuia hiyo adhabu? Jueni! Siku itakapo wajia basi haitoondolewa hiyo
kwao. Na yatawazunguka yale waliyo kuwa wakiyafanyia mzaha.
Basi labda utaacha baadhi ya yale yaliyo funuliwa kwako, na kifua kitaona dhiki
kwa hayo, kwa sababu wanasema: Mbona hakuteremshiwa khazina, au wakaja naye
Malaika? Wewe ni mwonyaji tu, na Mwenyezi Mungu ndiye Mlinzi wa kila kitu.
Na wasipo kuitikieni, basi jueni ya kwamba (hii Qur'ani) imeteremshwa kwa ujuzi
wa Mwenyezi Mungu, na kwamba hapana mungu ila Yeye. Basi je! Nyinyi ni Waislamu?
Basi je, mtu aliye na dalili wazi itokayo kwa Mola wake Mlezi, inayo fuatwa na
shahidi anaye toka kwake, na kabla yake kilikuwa Kitabu cha Musa kilicho kuwa
mwongozi na rehema - hao wanamuamini, na anaye mkataa katika makundi, basi Moto
ndio pahala pa miadi yao. Basi usiwe na shaka juu ya hayo. Hii ni Haki itokayo
kwa Mola wako Mlezi; lakini watu wengi hawaamini.
Na nani aliye dhaalimu mkubwa kuliko yule anaye mzulia Mwenyezi Mungu uwongo?
Hao watahudhurishwa mbele ya Mola wao Mlezi, na mashahidi watasema: Hawa ndio
walio mtungia uwongo Mola wao Mlezi. Laana ya Mwenyezi Mungu iwapate walio
dhulumu,
Na wakasema wakuu walio kufuru katika kaumu yake: Hatukuoni wewe ila ni mtu tu
kama sisi, wala hatukuoni wamekufuata ila wale walio kuwa kwetu watu duni, wasio
kuwa na akili. Wala hatukuoneni kuwa mna ubora wowote kutushinda sisi. Bali tuna
hakika nyinyi ni waongo.
Akasema: Enyi watu wangu! Hebu fikirini! Ikiwa mimi ninayo hoja wazi iliyo toka
kwa Mola wangu Mlezi, na amenipa rehema kutoka kwake, nayo ikakufichikieni; je,
tukulazimisheni kuikubali hali nyinyi mnaichukia?
Na enyi watu wangu! Mimi sikuombeni mali kwa ajili ya haya. Mimi sina ujira ila
kwa Mwenyezi Mungu; na mimi sitawafukuza walio amini. Hakika wao watakutana na
Mola wao Mlezi, lakini mimi nakuoneni mnafanya ujinga.
Wala sikwambiini kuwa nina khazina za Mwenyezi Mungu; wala kuwa mimi najua mambo
ya ghaibu; wala sisemi: Mimi ni Malaika. Wala siwasemi wale ambao yanawadharau
macho yenu kuwa Mwenyezi Mungu hatawapa kheri - Mwenyezi Mungu anajua yaliomo
katika nafsi zao - hapo bila ya shaka ninge kuwa miongoni mwa wenye kudhulumu.
Wala nasaha yangu haikufaini kitu nikitaka kukunasihini, ikiwa Mwenyezi Mungu
anataka kukuachieni mpotee. Yeye ndiye Mola wenu Mlezi; na kwake mtarejeshwa.
Na akawa anaunda jahazi, na kila wakipita wakuu wa kaumu yake wakimkejeli. Yeye
akasema: Ikiwa nyinyi mnatukejeli na sisi tunakukejelini kama mnavyo tukejeli.
Hata ilipo kuja amri yetu, na tanuri ikafoka maji, tulisema: Pakia humo wawili
wawili, dume na jike, kutoka kila aina, na ahali zako, isipo kuwa wale ambao
imekwisha wapitia hukumu; na watu walio amini. Na hawakuamini pamoja naye ila
wachache tu.
Na akasema: Pandeni humo kwa Bismillahi, Kwa Jina la Mwenyezi Mungu, kwenda
kwake na kusimama kwake. Hakika Mola wangu Mlezi ni Mwenye kusamehe Mwenye
kurehemu.
Ikawa inakwenda nao katika mawimbi kama milima. Na Nuhu akamwita mwanawe naye
alikuwa mbali: Ewe mwanangu! Panda pamoja nasi, wala usiwe pamoja na makafiri.
Akasema: Nitakimbilia mlimani unilinde na maji. (Nuhu) akasema: Leo hapana wa
kulindwa na amri ya Mwenyezi Mungu ila aliye mrehemu mwenyewe. Na wimbi
likawatenganisha, akawa katika walio zama.
Na ikasemwa: Ewe ardhi! Meza maji yako. Na Ewe mbingu! Jizuie. Basi maji
yakadidimia chini, na amri ikapitishwa, na (jahazi) likasimama juu ya (mlima) wa
Al Juudiy. Na ikasemwa: Wapotelee mbali watu walio dhulumu!
Na Nuhu alimwomba Mola wake Mlezi: Ee Mola Mlezi wangu! Hakika mwanangu ni
katika ahali zangu, na hakika ahadi yako ni haki. Na Wewe ni Mwenye haki kuliko
mahakimu wote.
Akasema: Ewe Nuhu! Huyu si katika ahali zako. Mwendo wake si mwema. Basi
usiniombe jambo usio na ujuzi nalo. Mimi nakuwaidhi usije ukawa miongoni mwa
wajinga.
Nuhu akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Mimi najikinga kwako nisikuombe nisio na
ujuzi nalo. Na kama hunisamehe na ukanirehemu, nitakuwa katika walio khasiri.
Ikasemwa: Ewe Nuhu! Shuka kwa salama itokayo kwetu, na baraka nyingi juu yako na
juu ya watu walio pamoja nawe. Na zitakuwapo kaumu tutakazo zistarehesha, na
kisha zitashikwa na adhabu chungu itokayo kwetu.
Na kwa kina A'adi tulimtuma ndugu yao Hud. Akasema: Enyi watu wangu! Muabuduni
Mwenyezi Mungu! Nyinyi hamna mungu isipo kuwa Yeye. Nyinyi si chochote ila ni
wazushi tu.
Na enyi watu wangu! Muombeni msamaha Mola wenu Mlezi, kisha mtubie kwake.
Atakuleteeni mbingu zenye kunyesha mvua ya kumiminika, na atakuzidishieni nguvu
juu ya nguvu zenu. Wala msigeuke mkawa wakosefu.
Sisi tunasema: Baadhi katika miungu yetu imekusibu kwa baa. Akasema: Hakika mimi
namshuhudisha Mwenyezi Mungu, na nyinyi shuhudieni, ya kwamba mimi najitenga
mbali na hao mnao wafanya washirika,
Hakika mimi nimemtegemea Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wangu na Mola Mlezi wenu.
Hapana kiumbe yeyote ila Yeye anamwendesha atakavyo. Hakika Mola wangu Mlezi
yuko juu ya Njia Iliyo Nyooka.
Na ikiwa watarudi nyuma, basi mimi nimekwisha kufikishieni niliyo tumwa kwenu.
Na Mola wangu Mlezi atawaleta watu wengine badala yenu, wala nyinyi hamumdhuru
kitu Yeye. Hakika Mola wangu Mlezi ni Mwenye kuhifadhi kila kitu.
Na wakafuatishiwa laana katika dunia hii na Siku ya Kiyama. Basi tambueni
mtanabahi! Hakika kina A'adi walimkufuru Mola wao Mlezi. Na tambueni mtanabahi
kuwa hakika waliangamizwa kina A'adi, kaumu ya Hud.
Na kina Thamud tuliwapelekea ndugu yao Saleh. Akasema: Enyi watu wangu!
Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu ila Yeye. Yeye ndiye aliye kuumbeni
katika ardhi, na akakuwekeni humo. Basi mwombeni msamaha, kisha mtubu kwake.
Hakika Mola wangu Mlezi yupo karibu, anaitikia maombi.
Wakasema: Ewe Saleh! Hakika kabla ya haya ulikuwa unatarajiwa kheri kwetu. Je,
unatukataza tusiwaabudu waliyo kuwa wakiwaabudu baba zetu? Na hakika sisi tuna
shaka na wasiwasi kwa hayo unayo tuitia.
Akasema: Enyi watu wangu! Mwaonaje ikiwa ninazo dalili zilizo wazi kutokana na
Mola wangu Mlezi, naye akawa kanipa rehema kutoka kwake - je, ni nani atakaye
ninusuru kwa Mwenyezi Mungu nikimuasi? Basi nyinyi hamtanizidishia ila khasara
tu.
Enyi watu wangu! Huyu ngamia wa Mwenyezi Mungu ni Ishara kwenu. Basi mwacheni
ale katika ardhi ya Mwenyezi Mungu; wala msimguse kwa ubaya, isije
ikakuangamizeni adhabu iliyo karibu.
Basi ilipo kuja amri yetu tulimwokoa Saleh na wale walio amini pamoja naye kwa
rehema yetu kutokana na hizaya ya siku ile. Hakika Mola wako Mlezi ndiye Mwenye
nguvu Mwenye kushinda.
Wakasema: Je, unastaajabia amri ya Mwenyezi Mungu? Rehema ya Mwenyezi Mungu na
baraka zake ziko juu yenu, enyi watu wa nyumba hii! Hakika Yeye ndiye Msifiwa wa
kutukuzwa.
Wakamjia kaumu yake mbio mbio. Na kabla ya haya walikuwa wakitenda maovu. Yeye
akasema: Enyi watu wangu! Hawa binti zangu, ndio wametakasika zaidi kwenu. Basi
mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi mbele ya wageni wangu. Hivyo, hamna hata
mtu mmoja miongoni mwenu aliye ongoka?
(Wajumbe) wakasema: Ewe Lut'! Sisi ni wajumbe wa Mola wako Mlezi. Hawa
hawatakufikia. Na wewe ondoka pamoja na ahali zako usiku ungalipo. Wala yeyote
miongoni mwenu asitazame nyuma, isipo kuwa mkeo, kwani yeye utamfika msiba
utakao wafika hao. Hakika miadi yao ni asubuhi. Je, asubuhi si karibu?
Na kwa watu wa Madyana tuliwatumia ndugu yao Shua'ib. Akasema: Enyi watu wangu!
Muabuduni Mwenyezi Mungu. Nyinyi hamna Mungu ila Yeye, wala msipunguze vipimo na
mizani. Mimi nakuoneni mmo katika hali njema, nami nakukhofieni adhabu ya Siku
kubwa hiyo itakayo kuzungukeni.
Wakasema: Ewe Shua'ibu! Ni sala zako ndizo zinazo kuamrisha tuyaache waliyo kuwa
wakiyaabudu baba zetu, au tuache kufanya tupendavyo katika mali zetu? Ama hakika
wewe ni mstahamilivu kweli na mwongofu!
Akasema: Enyi watu wangu! Mwaonaje ikiwa ninayo dalili wazi inayo tokana na Mola
wangu Mlezi, na ikawa Yeye ameniruzuku riziki njema kutoka kwake? Wala mimi
sipendi kukukhalifuni nikafanya yale ninayo kukatazeni. Sitaki ila kutengeneza
kiasi ninavyo weza. Na sipati kuwezeshwa haya ila na Mwenyezi Mungu. Kwake Yeye
ninategemea, na kwake Yeye naelekea.
Na enyi watu wangu! Kukhalifiana nami kusikupelekeeni hata mkasibiwa kama
walivyo sibiwa watu wa Nuhu, au watu wa Hud, au watu wa Saleh. Na watu wa Lut'
si mbali nanyi.
Wakasema: Ewe Shua'ibu! Mengi katika hayo unayo yasema hatuyafahamu. Na sisi
tunakuona huna nguvu kwetu. Lau kuwa si jamaa zako tunge kupiga mawe, wala wewe
si mtukufu kwetu.
Akasema: Enyi watu wangu! Kwani jamaa zangu ni watukufu zaidi kwenu kuliko
Mwenyezi Mungu? Na Yeye mmemueka nyuma ya migongo yenu! Hakika Mola wangu Mlezi
ni Mwenye kuyazunguka yote mnayo yatenda.
Na enyi watu wangu! Fanyeni mwezayo, na mimi pia ninafanya. Karibuni mtajua ni
nani itakaye mfikia adhabu ya kumhizi, na nani aliye mwongo. Na ngojeni, mimi
pia ninangoja pamoja nanyi.
Na ilipo fika amri yetu, tulimwokoa Shua'ibu na wale walio amini pamoja naye kwa
rehema yetu. Na ukelele uliwanyakua walio dhulumu, na wakapambaukiwa majumbani
mwao wamekufa kifudifudi!
Na Sisi hatukuwadhulumu, lakini wao wenyewe wamejidhulumu. Na miungu yao waliyo
kuwa wakiiomba badala ya Mwenyezi Mungu haikuwafaa kitu ilipo kuja amri ya Mola
wako Mlezi. Na hiyo miungu haikuwazidishia ila maangamizo tu.
Na ama wale walio bahatika, wao watakuwamo Peponi wakidumu humo muda wa kudumu
mbingu na ardhi, isipo kuwa apendavyo Mola wako Mlezi. Hicho ni kipawa kisio na
ukomo.
Basi usiwe na shaka juu ya wanayo yaabudu hao. Hawaabudu ila kama walivyo abudu
baba zao zamani. Na hakika Sisi tutawatimilizia fungu lao bila ya kupunguzwa.
Na kwa yakini tulimpa Musa Kitabu; zikazuka khitilafu ndani yake. Na lau kuwa si
neno lilio kwisha tangulia kutoka kwa Mola wako Mlezi, bila ya shaka ingeli
hukumiwa baina yao. Na hakika wao wamo katika shaka juu yake inayo wahangaisha.
Basi, simama sawa sawa kama ulivyo amrishwa, wewe na wale wanao elekea kwa
Mwenyezi Mungu pamoja nawe; wala msikiuke mipaka. Hakika Yeye anayaona yote
myatendayo.
Basi mbona hawakuwamo katika watu wa kabla yenu wenye vyeo na wasaa wanao kataza
uharibifu katika nchi, isipo kuwa wachache tu, ambao ndio tulio waokoa? Na walio
dhulumu walifuata starehe zao, na wakawa ni wakosefu.